Monday, June 2, 2014

SEMANTIKI NA PRAGMATIKI



SEMANTIKI NA PRAGMATIKI


MAARIFA YA LUGHA NA MAARIFA YA ULIMWENGU

IMEANDALIWA NA MUBARAKA A HAMAD
CHUO KIKUU CHA DAR ES SALAAM

 Maarifa ya lugha ni elimu ya kupambanua vijengo mbalimbali vya lugha na kanuni zake kulingana na taratibu za lugha hio. Ulimwengu halisi ni mukatadha ambao maarifa ya lugha huweza kutumika ili kuleta taathira kama ilivyokusudiwa na msemaji au mwandishi.

Richmond Thomason (2012) anafafanua maana ya semantiki kwamba ni tawi la isimu ya lugha linalohusu maana za viyambo vya lugha. Hivyo basi ni kusema kuwa, semantiki ni utanzu wa isimu unaojishughulisha na maana ya maneno au viyambo vya maneno katika lugha. Swali kuu katika wanasemantiki ni kuhusu ninini maana ya maana. 

Hata hivyo wanasemantiki hujikita katika kuchunguza maana katika viwango mbalimbali kama vile; ngazi ya sauti (fonimu), neno, virai, vishazi na hata sentensi. Tawi hili la isimu limekuwa ni muhimu sana hasa kutokana na umuhimu wa mazungumzo, kwani ili mazungumzo yaeleweke na ujumbe ufahamike panahitajika maana. Aidha  nivyema ifahamike kuwa semantiki inajihusisha na maana za maneno kiisimu, kwani maana yake hupatikana kutokana na muundo wa maneno hayo au maarifa ya lugha husika.

Kwa upande wa pragmatiki Richmond Thomason (2012), anasema kwamba ni tawi la lugha linalojihusisha na matumizi ya lugha kwa kuzingatia muktadha wa wazungumzaji walugha husika. Hivyo Thomson anadai kuwa pragmatiki inahusu zaidi mambo mawili; matumizi na muktadha.
 
Geoffrey Finch (2000) anasema kuwa, dhana ya pragmatiki ilivumbuliwa katika miaka ya 1930 na mwanafalsafa C.W. Morris, na imeanza kujulikana kama tawi tegemezi la isimu lugha miaka ya 1970 ambapo kabla ya hapo pragmatiki ilihusishwa kama tawi la kifalsafa, na kufafanuliwa kwa kuzingatia misingi mikuu miwili; matumizi na muktadha.

Kuanazia miaka ya 80 wataaklamu walianza kuiangalia pragmatiki kama maana ya msemaji na tafsiri kilichosemwa, yaani maana ya msikilizaji. Kwa upande wake Yule (1996) anafafanua dhana ya pragmatiki kwa kusema kuwa ni taaluma inayohusu mahusiano yaliyopo kati ya maana ya lugha na watumiaji wa mambo hayo.

 Betty J. Birner (2012) anasema kuwa dhana hizi ni dhana zinazoshabihiana. Tofauti kubwa iliyopo kati ya dhana hizi bado ni mjadala mpana kwa baadhi ya wanaisimu wa lugha, hii ni kwa sababu, pragmatiki na semantiki zinajishughulisha na maana, kwa hio zipo hisia za ukaribu mno katika taaluma hizi mbili, licha kwamba pia zipo hisia za karibu za kuonesha utofauti wao.

 Niukweli usiopingika kwamba kuna maarifa ya lugha na wakati huohuo kuna maarifa ya ulimwengu halisi, hii inamaana kuwa kufahamu lugha peke yake haitoshi lazima lugha hiyo itumike kulingana na muktadha au ulimwengu halisi ambapo lugha hio imetumika. Hali hii inaweza kuthibitishwa kutokana na kuwepo kwa matumizi ya maana tofauti kwa kadri ya watumiaji husika kama ifuatavyo.

 Matumizi ya maana ya msingi katika kufafanua maana. Hii ndiyo njia kuu ya kulipa neno maana,  ambayo kwa kawaida haibadiliki kutegemeana na athari za kimazingira. Hii inamaana kuwa maana ya neno au tungo itabaki ile ile hata kama mazingira yatabadilika. Maaaana hii ndiyo inayojulikana kama maana ya kileksika. Kwa mfano; kichwa- kikimaanisha sehemu muhimu katika mwili wa binaadamu kinachokusanya viungo kama vile; macho, masikio, pua na mdomo. Hii ndiyo maana pekeyake inayohitaji ulimwengu wa lugha kwa kiwango kidogo sana, hata hivyo bado ulimwengu halisi utahitajika kutokana na matumizi ya maneno kama vile homophoni na homonimia. Mfano neno kama kaa licha ya kuwepo kwa maarifa ya lugha  lakini bado maarifa yaulimwengu halisi yanahitajika kuelewa kusudio la mzungumzaji, kwani yapo mazingira ambayo neno hilo litaendelea kutumika kama kitendo cha kuketi, na mazingira mengine litumike kama cheche la moto, na yote hayo ni maana ya msingi ya neno kulingana na miktadha tofauti tofauti.

 Maana ya ziada au kisarufi. Ni maana abayo huibuka kutokana na maana ya msingi. Maana hii inatudhihirishia kuwepo kwa maarifa ya lugha na wakati huohuo kuna maarifa ya ulimwengu halisi. Hii ni kutokana na ukweli kwamba, maana hizi hutegemeana na kuhusiana na mazingira halisi ya matumizi. Kuelewa maana ya ziada sio tu kuelewa maarifa ya lugha, bali pia ulimwengu halisi au muktadha ambapo maneno au fahiwa hizo zimetumika. Mfano pale mzungumzajia atakapo sema “Samahani kaka! Hivi utaendelea kuwa kupe hadi lini? haya ni maisha tu!” utagundua kuwa, hapa kufahamu maana ya tungo hii si kutokana tu na kufahamu maarifa ya lugha, lakini pia inahitajika ufahamu wa ulimwengu halisi ambao tungo hio imetumika, kwa kusema kupe kumaaanisha mtu mnyonyaji au mtegemezi.

Maana ya kimtindo. Hii ni maana inayohusiana moja kwa moja na matumizi ya lugha kulingana na muktadha husika. Katika aina hii ya maana, neno au kiyambo hupata maana kulingana na mtindo ambao neno au kiyambo hicho kimetumika. Mfano mtindo wa kilahaja, mtindo wa wakati, mtindo wa kieneo, au hata mtindo wa taaluma ua fani fulani. Ni lazima tukiri kwamba kuna marifa ya lugha lakini wakati huo huo kuna ulimwengu halisi. Hii ni kwa maana kwamba katika maana hii, lazima mtumiaji wa lugha licha ya kufahamu maarifa ya lugha hio, lakini lazima azingatie ulimwengu halisi ambao lugha hio imetumika. Mfano matumizi ya mtindo wa kilahaja, kuna baadhi ya maneno kiuhalisia huibua hisia zingine na wakati mwingine kushindwa kufahamika kutokana na tofauti za kilahaja. Mfano maneno kama vile, shule, ugali na bomba, maneno haya yanaweza kutumika katika hali tofauti kwa wakaazi wa Tanzania bara na visiwa vya Zanzibar. Kwa upande wa Zanzibar wangeweza kutumia skuli, sembe na mfereji kwa mfuatano. Hivyo basi, kwa mzungumzaji inampasa kujua ni akina nani anazungumza nao na nani wangeweza kumuelewa ingawa wate wana maarifa ya lugha moja.
Aidha, kuwepo kwa maana hisia ni ithibati tosha ya kuthibitisha kuwepo kwa maarifa ya lugha na wakati huohuo ulimwengu halisi katika dhana ya semantiki na pragmatiki zinazohusu maana. Tunapozungumzia maana  ya hisia ni aina ya maana ambayo huibuka kutokana na hisia au mtazamo wa msemaji au mwandishi. Na maana hii huweza kuwasilishwa kwa njia mbalimabali zikiwemo, njia ya maana kama dokezi au njia isiyo ya moja kwa moja. Kwa mfano “kweli wewe ni kidume wa mbegu kwelikweli!” katika tungo hii ni vigumu kufahamu mzungumzaji amemaanisha nini ikiwa msikilizaji hatohusisha maana au kauli hii na ulimwengu halisi au muktadha ambao msemaji au mwandishi amezungumza au kukusudia, kwani maana ya msemaji itakua tofauti na maana ya msikilizaji atakayojengwa kwa kuzingatia tu maarifa ya lugha. Mathalani hapa tunaweza kusema kuwa, msemaji amekusudia huyu kijana ni mchapakazi kwelikweli. Au kwa waswahili wanakawaida ya kumsifia mtu kwa kusema kwa mfamo, huyu mchezaji yaani hafai, mshenzi kwelikweli! Kiuhalisia neno hafai linamaanisha hali hasi ya mtu, vile vile mshenzi ni neno linalotaswira mbaya ya ufedheheshaji, lakini waswahili husema hivyo kuonesha sifa njema za mtu, tofauti n auhalisia. Hivyo kwa mtu kufasiri maana kulingana na maarifa ya lugha inapelekea kupotosha maana iliyokusudiwa.

Maana tangamani. Hii ni maana inayopatikana kutokana na matumizi ya lugha kulingana na muktadha husika wa matumizi kwa kuzingatia maana ya maneno mbalimbali na jinsi yanavyotumiwa kwa pamoja ili kuleta maana iliyokusudiwa. Maana hii pia inatuthibitishia kuwepo kwa maariufa ya lugha na wakati huohuo ulimwengu halisi. Hii inamana kuwa si kujua tu maariufa ya lugha ndio kuweza kuitumia lugha hio, lakini ni kwa vipi lugha hio ingeweza kutumika. Kwa mfano kauli kama vile “Mabibi na mabwana”, mvulan amtanashati, dada mrembo. Ukichunguza tungo hizi utagundua kuwa si kufahamu tu maarifa ya lugha, bali lazima mtumiaji afahamu ulimwengu halkisi wa matumizi ya maneno hayo. Mfano msemaji angeweza kusema, ‘mabibi na mababu” au “dada mtanashati” na ‘mvulana mrembo” jambo ambalo lisengekubalika kajika jamii za waswahili.

Maana mangwi au akise. Ni aina ya maana ambayo huibuka katika hali ambayo maana moja hukonyeza maana nyingine na hivyo humfanya mtu afikirie maana nyingine pia. Mfano kauli “naenda kujisaidia” Katik tungo hii inahitaji mtumiaji wa lugha au msikilizaji kufahamu ulimwengu halisi, yaani  wanajamii fulani wanavyosema kujisaidia wanamaanisha nini? Kwa mfano mara nyingio katika jamii za kiafrika kujisaidia humaanisha ima kuenda haja ndogo au kubwa. Jambo hili katu lisengefahamika kwa sababu tu ya kufahamu maariga ya lugha hio.

Mwisho ni maana ya dhamira au muhimu. Hii ni aina ya maana ambayo hutegemea kile ambacho mtoa ujumbe ana kipa umuhimu zaidi. Mara nyingi kile kinachopewa umuhimu zaidi hutokeza mwanzoni mwa senmtensi. Msingi wa kupata maana katika aina hii inathibitisha kuwa pamoja na kuwa na marifa ya lugha pia panakuwepo n aulimwengui halisi wa lugha. Kupitia aina hii ni vigumu mtu kutambua umuhimu wa msemaji au mzungumzaji kwa msingi tu wa maarifa ya lugha bila kuhusisha hali gani lugha hio imetimika. Mfano kauli ya kusema “Kikwete atashinda uchaguzi wa mwaka 2015” Katika mfano huu umuhimu zaidi upo kwa Kikwete ndiye ambaye ana tarajiwa kushindsa uchaguzi na sio uchaguzi wala mwaka 2015. Haya yote yatabainika ikiwa tu msikilizaji atakuwa anamaarifa ya lugha na wakati huohuo anaujua ulimwegu halisi.

Kwa kuhitimisha tunaweza kusema kuwa,  semantiki na pragmatiki zote kwa pamoja zinahusiana, kwa mana kwamba zinajihusisha na maana ya maana katika lugha. Wala haitokuwa sahihi kudhani kwamba kufahamu tu maana ya viambajengo katika tungo, iwe neno, kirai, kishazi au hata sentensi kuwa ndio kufahamu kwa kile kilichokusudiwa   bila kujali muktadha ambao neno hilo imetumika.  

 Hat hivyo, taaluma hizi bado zitaendelea kuwa tofauti kwa kuwa semantiki hujihusisha na maana za maneno au viyambo vya maneno kama vilivyo kupitia kwa masemaji na msikilizaji. Wakati huohuo pragmatiki hujishughulisha  na jinsi gani muktadha unapelekea kupata maana ya kile kilichokusudiwa kulingana na muda mahsusi. 

Aidha ifahamike kuwa Semantiki na Pragmatiki zote kwa pamoja zimelenga kutoa ufafanuzi  kuhusu mchakato wa lugha na matumizi yake kulingana na muktadha wa uzungumzaji au utumikaji wake. Kama sehemu ya mfumo wa mazungumzo , sambamba na kufasiri na kufafanua mfumo fungamanifu wa  mazungumzo katika lugha, na hili litafikiwa tu kwa kuzingatia maarifa ya lugha sambamba na ulimwengu halisi wa mazungumzo.












 MAREJEO.
Geoffrey Finch, (2000). Linguistic Terms and Concepts. Palgrave Macmillan.
Jacob L. Mey, (2001). Pragmatics: An Introduction, 2nd ed. Wiley-Blackwell.
 Richmond H Thomason (2012). What is semantics? Second version.
Wwww.wisegeek.com Publishing & Printing International Journal. (USA), downloaded on Friday, 30th May 2014, at 12:30 pm.
Yule, G. (1996). Pragmatics. Oxford: Oxford University Press.


8 comments: